Tuesday 11 October 2016

MSICHANA WA CHINI YA MIAKA 15 HUOZWA " KILA SEKUNDE SABA"




Save the Children: Msichana wa chini ya miaka 15 huozwa 'kila sekunde saba'
  • 11 Oktoba 2016



 India ni moja ya nchi ambazo zinaongoza kwa visa vya ndoa za watoto, ripoti hiyo inasema

Ripoti mpya ya shirika la Save the Children inasema msichana wa chini ya miaka 15 huozwa kila baada ya sekunde saba duniani.


Ripoti hiyo inasema watoto wa hadi chini ya miaka 10 wanashurutishwa kuolewa na wanaume wazee katika nchi kama vile Afghanistan, Yemen, India na Somalia.

Save the Children wanasema ndoa za mapema zinaweza kuchangia msururu wa matatizo ambayo huathiri maisha yote ya msichana.


Mizozo, umaskini na migogoro ya kibinadamu vinatazamwa kama sababu kuu zinazowaweka wasichana hatarini ya kuozwa wakiwa bado wana umri mdogo.


"Ndoa za mapema huanzisha msururu wa matatizo ambayo humnyima msichana haki za kimsingi za kujifunza, kujikuza na kujivunia maisha yake kama mtoto," amesema afisa mkuu mtendaji wa Save the Children International Helle Thorning-Schmidt.


"Wasichana wanaoolewa wakiwa wadogo mara nyingi huwa hawawezi kuendelea na masomo, mara nyingi hudhulumiwa na waume zao, kupigwa na hata kunyanyaswa kingono. Hupachikwa mimba na pia huwa hatarini ya kuambukizwa magonjwa ya zinaa, ukiwemo Ukimwi."


Ripoti hiyo iliyopewa jina Every Last Girl, imeorodhesha nchi ambazo ni ngumu zaidi kwa wasichana baada ya kuzingatia elimu, ndoa za watoto, mimba za mapema, vifo vya wanawake wakijifungua na idadi ya wanawake bungeni.


Chad, Niger, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Mali na Somalia zinashika mkia kwenye orodha hiyo.

Image copyright Getty Images Image caption Ripoti hiyo inasema wasichana kwenye kambi za wakimbizi wamo hatarini ya kuozwa wakiwa wadogo 


Shirika la Umoja wa Mataifa linalowashughulikia watoto, Unicef, linakadiria kwamba idadi ya watoto watakaoozwa wakiwa wadogo itaongezeka kutoka 700 milioni kwa sasa hadi 950 milioni kufikia 2030.

Ripoti hiyo ya Save the Children imetolewa siku ya maadhimisho ya Siku ya Msichana Duniani.

NDOA ZA UTOTONI JANGA TANZANIA



Ndoa za utotoni janga Tanzania
  • 29 Oktoba 2014

Image caption Watoto walioathirika na ndoa na mimba za utotoni Tanzania 



Tanzania ni moja ya nchi zinaoongoza kwa mimba na ndoa za utotoni, kwa mujibu wa ripoti inayotarajiwa kuzinduliwa hii leo jijini Dar es Salaam na Shirika la Haki za Binadamu duniani.

Hata hivyo nchi hiyo imepiga marufuku ndoa hizo, ambapo mtoto wa kike anaruhusiwa kuolewa anapofikisha umri wa miaka kumi na nane.


Mkoa wa Shinyanga ulio kaskazini magharibi mwa Tanzania ndio unaotajwa kuongoza kwa mimba na ndoa za utotoni, ikilinganishwa na mikoa mingine nchini humo.

Takwimu kutoka mashirika mbalimbali ikiwemo UNICEF zinaonyesha kuwa, kwa siku, watoto 16 wanapachikwa mimba za utotoni.


Kwa mujibu wa wataalamu, hali hii imekuwa ikiendelea kwa muda mrefu na kwa asilimia kubwa imezorotesha maendeleo ya mtoto wa kike katika eneo hilo.


Ili kumwokoa mtoto wa kike kutokana na janga hili, kumekuwa na jitihada mbalimbali kutoka mashirika yasiyo ya kiserikali za kuwaokoa hasa wale ambao tayari wameshatumbukia katika dimbwi hilo.

Shirika lisilo la kiserikali la Agape limeweza kuwaokoa wanafunzi wa kike wapatao mia mbili, wakiwa wamepitia ndoa za utotoni. Wengine tayari wamezalishwa wakiwa na umri chini ya miaka 13. Hivi sasa wanaanza maisha mapya ya kusoma.


Mmoja wa watoto waliokolewa akiwa amejitambulisha kwa jina la Pili Omar, ana miaka 14 na ni mama wa mtoto mmoja. na amekubali kueleza kilichomsibu."Niliolewa kwa sababu wazazi wangu waliniambia sitaendelea kuwa mzigo kwao, hivyo niolewe ili nianzishe mji wangu."anasema Pili.


Wazazi na walezi wa watoto hawa wanalaumiwa kwa kuwalazimisha watoto wao kuingia katika ndoa za utotoni. Licha ya kukithiri kwa ndoa hizo, pia imebainika kwamba asilimia 99 ya ndoa hizo hazidumu. Harieth Kulwa ni mmoja wa waathirika wa ndoa hizi ambaye ndoa yake imevunjika."Nilidhai kuolewa ndio kutatatua matatizo yangu, kumbe nilijiongezea matatizo. Mwanamume aliyenioa kwanza alikuwa mkubwa kwangu, pili alikuwa mlevi…" Anabainisha Harieth.


Hata hivyo, wanaharakati wa haki za binadamu wanaulalamikia mfumo mzima wa kusimamia sheria kwa kutowachukulia hatua kali za kisheria watu wanaobainika kuwasababishia mimba watoto, wakidai kuwa ni kutokana na vitendo vya rushwa vilivyogubika vyombo vya shERIA.

 BBC  SWAHILI

UKATILI WA KIJINSIA BADO NI KIKWAZO NCHINI TANZANIA



Ukatili wa kijinsia bado ni kikwazo nchini Tanzania
  • 19 Agosti 2016

Tanzania inakabiliwa na kiwango cha juu cha ukatili wa kijinsia ikiwemo ndoa na mimba za utotoni, pamoja na vipigo kwa wanawake kutoka kwa waume zao licha ya juhudi mbali mbali za kupinga hatua hiyo na sheria kali kutungwa bado matukio ya aina hii yanazidi kuongezeka.


Utafiti wa hali ya afya ya uzazi,mtoto na malaria wa mwaka 2015/2016 unaonesha kuwa idadi ya wasichana wanaopata watoto katika umri wa miaka 15-19 imeongezeka mpaka kufikia asilimia 27 mwaka 2015 kutoka asilimia 23 mwaka 2010.


Kwa muujibu wa utafiti uliofanywa na UNICEF wa mwaka 2015,Tanzania ina asilimia 3.5 ya watoto wa umri wa miaka 7-17 walio nje ya shule.

Hii inajumuisha watoto takriban milioni 2 walitakiwa kuwa shule za msingi na watoto takriban milioni 1.5 waliotakiwa kuwa shule za sekondari.


Aidha utafiti huo umetanabahisha kuwa katika kila watoto watano wa umri wa kuwa shule ya msingi,kuna mtoto ambaye hayuko shuleni na katika kila watoto watano wa umri wa kuwa shule ya sekondari kuna watoto zaidi ya wawili ambao hawako shuleni kutokana na sababu mbali mbali.


Katika  harakati  za   kutokomeza   ndoa  za  utotoni ,ukatili wa kijinsia kwa mtoto wa kike na wanawake licha ya kuwapa mafunzo maafisa maendeleo ya jamii ,maafisa ustawi wa jamii na hata polisi na kuwajengea uwezo wasichana ,vilabu 350 vya wasicha vimeundwa nchini Tanzania ambao wanatambua haki zao za msingi.

 BBC  SWAHILI